MFAHAMU SHAROE

Sharon Gwada ndilo jina analotumia sana. Hupenda kulitumia jina lake la kwanza na la mwisho kati ya majina yake manne. Sababu kuu ya kuyatema majina yake ya kati ni kuwa watu humtania kwayo. Pili, hujivuna sana anapowapa watu utata wa kujaribu kulitambua kabila lake. Kwa hivyo, itakubidi utokwe kijasho kabla ya kuyang’amua yote manne.

Sharon ni binti mrembo sana mwenye umri wa miaka ishirini na mitatu. Urefu wake ni futi 5.8, mweusi mwenye haiba ya kuvutia na kunasa makini ya madume. Mrembo huyu ni bashashi na ambaye ucheshi wake humfikisha kwenye kilele cha kucheka sana kila inapobidi.

Ni ashiki mkubwa wa kusoma anayejibidiisha kusoma walau sura moja ya kitabu kila siku. Anapenda zaidi kusoma kazi za fasihi za kiafrika. Kwa sasa, anapania kusoma angalau kitabu kimoja kutoka kila taifa duniani. Sijakueleza kuwa Sharon ni mwandishi vile vile? Haya basi, binti huyu huandika kuhusu matukio hai ya maishani na kufanya machapisho yake kwenye blogu yake;

http://underratedblogger.com

Kinaya kilichopo ni kuwa, huba yake humwelekeza kusoma kazi za fasihi bunifu, ilhali anapoandika, hutilia maanani matukio hai.

Binti wa watu hakosi kulificha penzi alilo nalo kwa kiwiliwili chake anachokitunza kwa uta na upote. Hukoga hata ikibidi mara kumi kwa siku, akavalia nadhifu na kujiweka sawa. Kwa ajili hii, huviona paa vyakula vinavyoleta hatari kwa afya na hukumbatia lishe bora kila wakati.

Jambo kuu linalomwogopesha dada huyu ni kupatwa na maradhi ya namna yoyote. Hata anapoemewa na mafua, hufanya lolote yamwondokee haraka iwezekanavyo. Anachukia dawa, anachukia hospitali, anayachukia mazingira yoyote ya matibabu na harufu inayoambatana na maeneo hayo. Nimekuambia kuhusu asivyoweza kustahimili mtazamo wa sindano za hospitali? Haliwezi hili kamwe wala hakumbuki mara ya mwisho alipochomwa na kifaa hiki. Vile vile, binti huyu anachukia kwa dhati yake yote wazo la kulazwa kitandani kwa ajili ya maradhi. Hili pekee huweza kumvuruga likamtoa uhai hata badala ya maradhi yenyewe.

Sharon amekwisha kuhitimisha masomo yake katika taaluma ya uanahabari. Anayo shahada kutoka chuo kikuu cha kiufundi cha Mombasa. Bado hajapata ajira na anajishughulisha na uandishi ili angalau apate tonge. Vile vile, hufanya mauzo ya mtandaoni, akiutumia mtandao wa kijamii wa ‘twitter’. Anaiona nyota yake ya uanahabari ikijongea, na hasa sana, itakuwa fahari kubwa kwake kuyaonyesha makeke yake kwenye runinga.

Ni kiongozi aliyewajibishwa na ‘The Writers Guild Kenya’ kunoa na kukuza vipaji vya waandishi wa mkoa wa pwani. Vikao vyao hufanyika jijini Mombasa kila Ijumaa kuanzia saa nane za mchana.

Miongoni mwa vitu anavyopenda ni;
1) Kufanya matembezi na kuzuru maeneo mapya
2) Kupika (hasa chapati)
3) Kuhudhuria makongamano na hafla za burudani
4) Kujifunza mambo mapya
5) Kutizama filamu
6) Kusikiliza mziki

Baadhi ya vitu asivyovipenda ni kama ifuatavyo;
1) Kukosa kutimiza malengo yake
2) Kushindwa kutoa msaada kwa mtu aliye na uhitaji
3) Kukosa hela na kuhitajika kukopa ili kutimiza matakwa yake

Chakula anachokienzi kwa dhati ni chapati. Anazipenda chapati kwa kuwa ati ni mpishi hodari wazo. Vile vile, anapenda sana vyakula vya kiswahili vilivyopikwa na waswahili wenyewe kama vile biryani na pilau.

Ana chuki isiyopigiwa mfano kwa mboga za majani. Sababu kuu ni kuwa amezila sana maishani.

Anapenda rangi nyeusi kwa kuwa rangi hiyo huchukuana vizuri na rangi zingine. Haibagui…

Je, unataka tutoe maelezo kukuhusu ili upate kujielewa vizuri, ufahamike vyema kwa rafiki zako, kuweka kumbukumbu mtandaoni na kupata rafiki wengine? Nitumie ujumbe kwenye:

  • 254729673536

ama

  • hussaynqassym@gmail.com

Shukrani za dhati kwa kusoma!

©husni

Published by husni bongo pevu

Soma! Soma Tena! Tena Soma, Kisha Andika.

Join the Conversation

12 Comments

  1. Lugha yatatanisha kweli kwali lakini hakuna furaha ninayoipata kusoma maandisha yenye madaha kama hizi. Keep the great work. It was great relieving and reminiscing my fasihi fasaha again. Kila la heri kwa yote unayoifanya Sharoe.

    Liked by 1 person

  2. Lugha yatatanisha kweli kwali lakini hakuna furaha ninayoipata kusoma maandisha yenye madaha kama hizi. Keep the great work. It was great relieving and reminiscing my fasihi fasaha again. Kila la heri kwa yote unayoifanya Sharoe.
    ^Willian.

    Liked by 1 person

Leave a comment

This site uses Akismet to reduce spam. Learn how your comment data is processed.